Na RIPOTA WETU
Jumanne, Januari 21, 2025
TIMU ya wanaume ya Simlaw na Jacaranda kila moja ilionyesha voliboli ya kuvutia na kunasa tikiti ya fainali kuwania taji la Mtaa Cup kwenye mechi zilizoandaliwa eneo la Bahati, Kaunti ya Nairobi.
Mechi hizo zilizochezwa Jumapili, Januari 19, 2025 zilivutia jumla ya timu 16
kutoka mitaa tofauti hapa Nairobi ambapo timu hizo mbili zilinyanyasa wapinzani wao kwenye mechi za nusu fainali..
Shindano hilo liliandaliwa na klabu ya The Beast ambayo hushiriki ligi ya taifa daraja la kwanza. ”Tuliandaa shindano hilo kwenye juhudi za kutambua talanta za wana voliboli chipukizi mtaani ambao baadaye wanaweza kujiunga na timu za ligi kunoa vipaji vyao,” alisema Joseph Ochieng meneja wa The Beast. Aliongeza kuwa wataendelea kuandaa mechi sampuli hiyo ili kutoa nafasi kwa wachezaji wengi kushiriki maana siku zijazo ndiyo watakaofuzu kushiriki voliboli ya kimataifa.
Kwenye nusu fainali, Simlaw ilikung’uta Stars Kenya kwa seti 3-0 nayo Jacaranda ilisajili seti 3-1 dhidi ya The Beast. Katika robo fainali, The Beast iliadhibu Huruma kwa seti 3-0, Stars Kenya ilichapa Twigs Stars kwa seti 3-1, Kawangware ilipepetwa seti 3-0 na Simlaw huku Jacaranda ikitwaa ushindi wa seti 3-1 mbele ya Bahati.
Kwenye mechi za makundi timu hizo zilionyesha ushindano mkali na kujikatia tikiti za robo fainali. Katika jedwali ya mechi hizo Kundi A: Twigs Stars ilimaliza kifua mbele kwa alama tisa, tatu mbele ya The Beast. Kundi B, Jacaranda ilionyesha ubabe wake na kuzoa alama tisa, tatu mbele ya Kawangware. Vile vile Kundi C, Simlaw ilimaliza kidedea kwa alama tisa nayo Bahati ikiwa ya pili kwa kusajili pointi sita. Huruma iliyopangwa Kundi D iliibuka wababe kwa alama saba, moja mbele ya Stars Kenya.
Post Views: 531